October 31, 2014

WASAA WA MAZINGIRA UNUFAISHE JIJI LA ARUSHA

Arusha. Jiji la Arusha limeteuliwa kuwa ni kati ya majiji 7,000 duniani kushiriki shindano la wasaa wa mazingira linalolenga kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchini.
Kwa bara la Afrika, ni nchi mbili tu, ambazo zipo katika mpango huo, ambazo ni Tanzania na Afrika Kusini.
Mradi huu, ambao hapa nchini unaratibiwa na shirika la kimataifa la Mazingira (WWF), pia unalenga kupunguza tatizo la ongezeko la hewa ya ukaa duniani.
Katika mradi huu, Jiji la Arusha linapaswa kuongeza upandaji wa miti, kuongeza jitihada za usafi wa mazingira na kuanza mipango ya matumizi ya nishati mbadala.
Ofisa Nishati Jadidifu wa WWF, Philipina Shayo anasema Arusha ina fursa ya kubadilika kutokana na kuingizwa katika mradi huu.
Shayo anasema katika mradi huo, utakaofanyika katika nchi 18 duniani, miji ya Moshi na Dar es Salaam itanufaika.

Anasema mradi huu ni wa mitatu 2014-2016 ambao lengo lake ni kuchangia katika kutoa elimu endelevu katika matumizi ya nishati mbadala ili kupunguza tatizo la ongezeko la hewa ya ukaa na mabadiliko ya tabia nchi.
Mratibu wa program ya nishati jadidifu wa WWF, Dk Thelesia Olemako. Anasema Arusha ina bahati kubwa kuingizwa katika mpango huu.
Licha ya kutambuliwa kidunia katika vita dhidi ya athari za mabadiliko ya tabia nchi, pia itatajwa kuwa moja ya majiji ambayo yapo katika mpango wa kupunguza hewa ya ukaa.
Meya wa Arusha, Gaudence Lymo anasema jiji limejipanga kushiriki katika mradi huo, ili kukabiliana na matatizo ya tabianchi na ongezeko la hewa ya ukaa.
Lyimo anasema katika mradi huo wa Wasaa wa Mazingira, Jiji la Arusha, litajitahidi kuendelea kutunza mazingira kwa kupanda miti, kufanya usafi na kutunza mazingira licha ya ongezeko kubwa la watu kuwepo.
Naye mwenyekiti wa kamati ya ya huduma za jamii, Isaya Doita anaeleza mipango ya jiji itafanikiwa katika mradi huu.
Anasema hadi sasa miti zaidi ya milioni 3 imezalishwa na miti zaidi ya 500,000 inaendelea kupandwa maeneo mbalimbali ya jiji.
Hata hivyo anafafanua kuwa kufanikiwa kwa mradi huu pia kunasukumwa na ushirikiano baina ya wananchi, viongozi wa kisiasa na wakuu wa idara.
Ofisa wa afya wa jiji, James Lobikoki anasema kukamilisha ujenzi wa jalala la kisasa, ujenzi uliogharimu kiasi cha Sh4.3 milioni, ni nafasi ya kufanya vizuri katika mashindano haya.
Anasema dampo hilo, ambalo kwa siku linapokea tani 385 za taka, linasaidia sana kupunguza tatizo la kusambaa kwa taka mbalimbali katika jiji hilo.
Kauli za viongozi hawa wa jiji na WWF zinapaswa kuwa ni faraja kwa jiji. Anasema hata kama Arusha haitashinda kuwa kati ya majiji bora duniani, wananchi watanufaika.
Fursa hii inapaswa kutumika, kusaidia jiji la Arusha kuboresha miradi ya mazingira ya upandaji miti, uanzishwaji wa kiwanda cha kusaga taka na kutengeneza mkaa ili miti isikatwe na pia kutumika dapo kuzalisha umeme.
Kuingizwa kwa Jiji la Arusha katika mpango huu, pia kutasaidia kuanzishwa miradi ya umemejua sambamba na matumizi ya vifaa visivyotumia umeme mkubwa. Hali kadhalika kutawezesha maeneo ya pembezoni kusaidiwa miradi ya nishati jadidifu ili kuachana matumizi ya nishati kubwa ya umeme.
Jiji la Arusha pia linapaswa kusaidiwa kuwa na mradi kabambe wa kuhakikisha miradi ya kukusanya taka inaimarishwa, mpango wa ukusanyaji maji taka unaboreshwa na pia kufukuliwa mifereji ya asili ya majitaka.
Zamani, Arusha ilikuwa ni jiji la baridi, mito ya maji safi, kama Naura na Ngarenaro, ilikatisha katikati ya jiji, lakini sasa imegeuka maeneo ya kutupa taka na maji yamebaki ni historia.
Hivyo ni matumaini ya wengi mradi wa wasaa wa mazingira, utalinufaisha Jiji la Arusha kurejea katika uhalisia wake na hivyo kupungua kwa joto, na kuongezeka kwa mvua.



Chanzo cha Habari ~Mwananchi~

No comments:

Post a Comment